Saturday, June 27, 2015

UMASKINI WA TANZANIA: SABABU MBADALA ZA UMASKINI WETU



DIBAJI

Kumekuwa na maelezo na sababu nyingi zinazotolewa kuhusu umaskini wa jamii ya Tanzania. Wako wanaosema kukosekana kwa uwekezaji ni chanzo kikubwa cha uchumi wetu kuyumba.

Lakini katika kuvutia uwekezaji huo, lazima tujiulize, je fursa zinazojitokeza za kiuchumi zina uwezo wa kubadilisha uchumi wetu kutoka katika hali duni?

Changamoto nyingine inayosemwa ni juu ya Teknolojia. Je teknolojia hii hasa hasa ya kutoka nje inasaidia uchumi wetu kukua? Na kama ni hivyo ukuaji wake una changamoto gani?

Changamoto za elimu, mathalani ni elimu gani ambayo inatolewa na ina manufaa gani kwa umma?

Lakini pia, hatudhani kuwa kuna matatizo au sababu nyingine ambazo zinachangia suala zima la umaskini wa Tanzania na kuwa ni sababu hizi tunaishi nazo na ni sehemu ya kawaida ya maisha ya watu?

Kupitia kitabu hiki nitajitahidi kuainisha sababu mbadala za Tanzania na Watanzania kuwa maskini katika nchi yenye utajiri mwingi wa mali asili kuliko nchi nyingi zilizoendelea.



SURA YA KWANZA
MATUMIZI YA LUGHA ISIYO YA ASILI KWA MTANZANIA -
KISWAHILI

Kiswahili ni lugha sasa ya kimataifa. Ni lugha ambayo wengi hatuwezi tena kukataa kuwa ina mashiko kijamii na kimataifa na mikakati ni kuifanya iwe lugha kuu hapa Afrika. Wazo kama hili ni jema sana. Litaifanya Afrika iwe na lugha yake pekee ambayo imetokana na eneo la Afrika na ambayo imeweza kutumiwa na jamii pana.

Nchi ya Tanzania ina uzoefu mkubwa wa matumizi ya Kiswahili hasa kutokana na kuwa na pwani kubwa ya Afrika Mashariki, na inavyosemekana ndiyo imekuwa kiungo cha kuleta umoja na amani iliyopo leo. Wakati wa kupambana na wakoloni inasemwa Kiswahili kilikuwa nguzo moja wapo ya kuwaunganisha Watanganyika wakati huo. Na katika Mapinduzi ya Zanzibar, Kiswahili pia kilitumika kuwaunganisha Wazanzibar.

Kiswahili kina mengi sana ya sifa kama ilivyo kwa uwepo wa lugha nyingine duniani. Kusudi langu la kuandika kitabu hiki sio kueleza yale ambayo tayari yamekuwa yakielezwa kuhusu Kiswahili na umuhimu wake katika maisha yetu ya kila siku.

Bali, ni kuona namna lugha inavyoweza kuwa na athari pana katika maisha ya kila siku ya jamii inayoitumia. Kiswahili kinabeba dhana ya uswahili. Uswahili unabebwa na dhima ya Mswahili. Mswahili ni nani?


Tukijaribu kurudi nyuma katika maisha ya makabila mbalimbali na hasa yale kwa namna moja au nyingine yalitoa mchango katika kukitengeneza Kiswahili (makabila ya pwani) ambayo yalipata bahati kukutana katika shughuli mbalimbali za kijamii, na Waarabu tunapata kizazi kipya hiki cha Mswahili.

Kiswahili kimsingi kimechangiwa kwa karibu sana na Waarabu, Wahindi  na makabila mengi ya Pwani ya Afrika Mashariki. Makabila yetu ya pwani, Waarabu na Wahindi hawa kimsingi walijua lugha zao za asili, yaani lugha za makabila yao, kwa Waarabu - Kiarabu na kwa Wahindi - Kihindi. Wote hawa walishirikiana katika biashara, kuoleana na kadhalika. Katika kutafuta kuwasiliana, ndipo Kiswahili kikazaliwa.  Kimeendelea kupanuka kutokana na mwingiliano wa jamii nyingine za makabila na nchi nyingine ijapokuwa hakijapoteza ile dhima yake ya uswahili.

Jamii iliyozaliwa hapa ilitengeneza ustaarabu wa namna yao ya kuishi na kufanya shughuli zao za maendeleo. Kama ilivyokuwa Uarabuni kuna mafuta, na Pwani kuna mazao ya samaki yaani kuvua, pia pwani kuna mazao ya muda mrefu kama minazi, mikorosho na miembe, mwingiliano huu ukaleta ile dhana pwani shughuli nyingi zinasimamiwa na “uasilia” wa MAZINGIRA (Waarabu - Mafuta).

Je ni aina gani ya biashara au shughuli gani walizokuwa wanafanya? Na baada shughuli za uzalishaji mali ambazo kimsingi ni uchimbaji mafuta kwa Waarabu (na hapa hufanyika na makampuni sio mtu binafsi na kutokana na mazingira hakuna uzalishaji wa moja kwa moja wa shughuli nyingine – UKAME  wa jangwa) na kuvua kwa makabila ya pwani, basi walijipumzisha huku wakicheza michezo mbalimbali. Je mfumo wa michezo yao ulikuwa au ukoje mpaka leo?

Utamaduni uliozaliwa hapa ni ule wa kuitegemea asili (nature) ikupatie kile unachokitafuta. Kwa kuwa uwepo wa mafuta ni wa muda mrefu, vivyo hivyo kwa samaki katika bahari na maziwa, Mswahili aliyetengenezwa hapa alijikuta akiwa mtu mwenye kusubiri, kujenga matumaini ya kujua maisha yanaendelea hakuna tatizo. Utamaduni ambao jamii haina uwajibikaji wa moja kwa moja.

Alilima mazao yanayotoa mazao kwa muda mrefu kama minazi, korosho, maembe na kadhalika.

Hakuwa tayari kufanya shughuli ambayo kwake ni shulba na ambazo hata baada ya kuja kwa wazungu walipoambiwa wazifanye waliona adhabu kama kilimo cha katani na mazao mengine, utengenezaji wa miundo mbinu n.k.

Ndipo katika Kiswahili tunakutana na neno pole kwa kazi! Kwa sababu kazi haikuchukuliwa kama kitu chema, ni cha kuudhi na kinachofanywa na yule mwenye matatizo makubwa katika maisha yake. Asiye na matatizo hatakiwi kufanya kazi na akionekana ni alama tosha kuwa ana shida katika maisha yake.

Mfumo wa kufikiri kwa mtu aliyetokana na uswahili (Kiswahili kikiwa ndiyo msafirishaji wa maadili na teknolojia), hakuashirii msukumo wa uzalishaji katika kiwango cha juu bali kuwa mtu mwenye subira – “Subira yavuta heri”. Je ni kweli katika maendeleo tuwe na subira? Na je heri inatafutwaje?

Tunapozunguza leo, tukienzi Kiswahili ni lazima tukichunguze kwa makini pamoja na kuleta umoja na amani, je vitu hivi vimetupa manufaa gani? Ni yale yakutoona damu ikimwagika kutokana na matumizi ya silaha?

Je mbona damu nyingi zaidi inapotea kutokana na uvivu na uzembe unaofanywa na hao ambao wamekuzwa na Uswahili na Kiswahili na sababu kuu ni mfumo wa Kiswahili katika Maisha?   

Je, ni wangapi wanashindwa kutimiza ndoto zao kwa kukumbana na Uswahili katika utekelezaji wa majukumu yetu ya kila siku. Je, Uswahili unanasibishwa na nini; sio uvivu, uzembe, majungu, wivu unatokana na wengi kutopenda kazi hivyo kunyang’anyana kidogo kilichopo?


Je, ni kweli kuwa watanzania wengi hawana uwezo wa kushindana katika Afrika Mashariki kutokana na lugha ya Kiswahili au na tabia za Kiswahili na Uswahili? Je nchi nyingine jamii zinazozungumza Kiswahili wanachukuliwaje mathalani Burundi, Rwanda, Uganda na Kenya? Unapita sehemu fulani ya nchi unasikia “hapa ni kwa Waswahili”!! Wanakuwa na vigezo gani?

Ndipo sasa tunafikia suluhisho la kutafuta mfumo mwingine wa mawasiliano, usiotokana na Kiswahili, wenye asili ya kiafrika, unaweza kutoa picha ya msukumo wa asili yetu kufanya kazi kwa juhudi na kuwa na msukumo wa “performance”. Kuwa tunatamani kupata maendeleo, huku mfumo wetu hauna uasilia wa kimfumo kutusukuma kufanya kazi kwa weledi, kwa juhudi na maarifa.

Aidha, naomba tujadiliane kwa hoja ili tuone kama haya ninayoleta kwenu yana mashiko au laa! Na tufikie wote kuamua mustakabali wa taifa.

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.